Powered By Blogger

Translate

Thursday, July 18, 2013

MABOMBA YA GESI YAFIKA MTWARA


Mabomba maalu kwa ajili ya kusafirisha gesi 
Mtwara. Meli kubwa kutoka China tayari imetua katika Bandari ya Mtwara kwa ajili ya kushusha mizigo ya mabomba ya gesi ili kuanza kwa kazi ya ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam.
Mmoja wa watumishi ndani ya Bandari ya Mtwara ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini, alisema zaidi ya magari 20 yanatakiwa kupakua mzigo wa mabomba zaidi ya 4,000 kutoka bandarini hapo na kusafirishwa kwenda Kiranjeranje Lindi kwa ajili ya zoezi zima la ujenzi wa bomba hilo.
“Hayo magari mliyoyaona ni miongoni mwa zaidi ya magari 20 yanayokuja kupakua mzigo wa mabomba ambayo ni zaidiya 4,000 kwa ajili ya kuyapeleka maeneo mbalimbali ikiwemo Kiranjeranje Lindi kwa ajili ya kufanikisha zoezi la ujenzi wa njia ya kusafirisha gesi, upakiaji unaendelea hapa Mtwara na Dar meli inapakuwa mzigo ili kupelekwa kwenye maeneo husika na upakuaji kwa mikoa yote unaendelea kwa amani,” alisema.
Akizungumza na gazeti hili mmoja wa madereva wa magari maalumu kwa ajili ya kupakua mzigo wa mabomba,alisema wametokea Dar es Salaam na hii ni zabuni maalumu waliyoipata kwa ajili ya maandalizi ya kupokea mizigo na kupeleka yanakotakiwa hapo baadaye baadaye baada ya kukabidhiwa kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda.
“Hivi sasa tunaenda kupakiza mzigo kwa ajili ya maandalizi tukisubiri siku ambayo wahusika wakuu watakaokabidhiwa,ili na sisi tuanze zabuni yetu ya usafirishaji kuyapeleka yanakohitajika, “ alisema
Akizungumzia tukio hilo, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo Muhongo alisema tayari meli ilitua katika bandari ya Dar es Salaam na meli kubwa imetua Mtwara kwa ajili ya kushusha mzigo wa mabomba na watakapomaliza yatakabidhiwa na kupokewa kwa heshima kama alivyofanya waziri mkuu jijini Dar es Salaam juzi (Jumapili)
“ Kwa mtu anayejua uchumi kitu kitakachotutolea umaskini ni hii gesi, mimi ninashangaa watu wa Mtwara wahoji kwa nini mizigo mingine ishushwe Dare es Salaam badala ya Bandari yaMtwara, hata kwa barabara wengine wanaanzia Dar na wengine wanaanzia Mtwara halafu wanakutana, hivyo sioni sababu ya kusafirisha kwa magari baada ya kushusha mizigo yote Mtwara ni kwa nini tuharibu barabara ?” alihoji Profesa Muhongo.
Sudi Mohammedi alisema kitendo cha serikali kwenda kushusha mizigo mingine katika Bandari ya Dar es Salaam ni kuonyesha ni kwa kiasi gani viongozi wasivyoithamini Mtwara kwa kuiacha bandari hiiyo.
Kabla ya kupita kwa magari hayo ya kubeba mizigo maeneo ya Bima, vilianza vifaru vikifuatiwa na gari kubwa lililobeba wanajeshi lililokuwa likizunguka katika baadhi ya maeneo mbalimbali mkoani hapa.

MAOFISA WA WIZARA YA FEDHA MAHAKAMANI

Share bookmark Print Email Rating
 
0
Share
Dar es Salaam. Maofisa wawili wa Wizara ya Fedha wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi. Wanatuhumiwa kwa ufisadi wa fedha za utoaji wa matangazo na habari kwa vyombo mbalimbali vya habari.
Maofisa waliopandishwa kizimbani ni pamoja na Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi, Ernest Simon Mwakitalu na Ofisa Ununuzi, Liipu Neligwa ambao walisomewa mashtaka na Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Leonard Swai.
Wakati maofisa hao wawili wakipandishwa kizimbani na kusomewa mashtaka hayo, wengine wawili ambao walitakiwa kupandishwa kizimbani, Mkuu wa Kitengo cha Habari, Ingiahedi Mduma na Mkurugenzi wa Kampuni ya And- Line (2000) International, Daniel Ukwaya hawakuwapo mahakamani hivyo, mashtaka dhidi yao hayakusomwa hadi watakapokamatwa.
Washtakiwa hao wote kwa pamoja wanakabiliwa na jumla ya mashtaka 19. Shtaka moja ni kula njama kutenda kosa, mashtaka manane ya kutumia nyaraka za uongo ili kumdanganya mwajiri.
Mengine ni shtaka moja la matumizi mabaya ya madaraka, mashtaka manane ya kughushi, shtaka moja la ubadhirifu na shtaka moja la kusababisha hasara ya Sh19.8 milioni, ambalo ni shtaka mbadala kwa wote.
Akisoma hati ya mashtaka, Wakili Swai alisema washtakiwa hao walitenda makosa hayo kwa tarehe tofauti kati ya Juni na Julai, 2009.
Wakili Swai alidai kuwa washtakiwa hao walisaini hati za ununuzi zenye taarifa za uongo kwa lengo la kuonyesha kuwa Kampuni ya And Line (2000) International ilipewa fedha kwa ajili ya vipindi vinane vya matangazo katika vyombo vya habari vya redio, magazeti na runinga.
Alidai kuwa taarifa hizo kwenye vyombo vya habari zilihusu maonyesho ya 33 ya Biashara ya Kimataifa yaliyofanyika Dar es Salaam katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere, Kilwa Road, kuanzia Juni 28 hadi Julai 10, 2009, kwa thamani ya Sh19.8 milioni, jambo ambalo si kweli.
Baada ya kuwasomea mashtaka, Wakili Swai alisema upelelezi wa kesi hiyo umekamilika na kuiomba Mahakama ipange tarehe nyingine ya kutajwa ambayo washtakiwe wengine watakuwa wamekamatwa ili wasomewe maelezo ya awali kwa pamoja.
Washtakiwa waliokuwapo mahakamani jana walikana tuhuma dhidi yao na waliachiwa huru kwa dhamana baada ya kutimiza masharti ya kila mmoja kusaini hati ya dhamana ya Sh5 milioni, kuwa na wadhamini wawili wanaotambulika, ambao pia walisaini hati ya dhamana ya kiasi hichohicho.
Kesi hiyo iliahirishwa na Hakimu Mkazi, Nyigulile Mwaseba hadi Agosti 15, mwaka huu itakapotajwa tena.

HAPPY BITHDAY MANDELA

Share bookmark Print Email Rating
Raia wa Afrika Kusini akiwa na bango la kumtakia kheri ya siku ya kuzaliwa kwa Rais Mstaafu wa nchi hiyo, mjini Polokwane nchini humo. 
Johannesburg: “Happy birthday Mzee Madiba.” Rais wa kwanza na mzalendo wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, leo anatimiza umri wa miaka 95, pia anatimiza siku ya 40 tangu alipolazwa katika Hospitali ya Medclinic, Pretoria kwa ajili ya matibabu.
Nelson Rolihlahla Mandela, alizaliwa Julai 18, 1918 katika Kijiji cha Mvezo, eneo la Mthatha, Transkei Mkoa wa Eastern Cape na ametumia zaidi ya asilimia 70 ya maisha yake akipigania haki na usawa wa wananchi wa Afrika Kusini.
Maadhimisho ya miaka 95 tangu kuzaliwa kwa Mandela yanabeba uzito mkubwa kuliko maadhimisho mengine yaliyotangulia kwani kwa siku 40, wananchi wa Afrika Kusini wamekuwa katika wasiwasi mkubwa hasa kutokana na kuzorota kwa afya ya kiongozi huyo.
Mandela alilazwa katika hospitali hiyo Juni 8, mwaka huu akiugua magonjwa ya figo na afya yake imeelezwa kuwa ni mbaya.
Leo, Rais Jacob Zuma atawaongoza mamilioni ya wananchi wa Afrika Kusini katika maadhimisho ya nne ya kimataifa ya ‘Siku ya Mandela’ ambayo yanakwenda sambamba na siku yake hiyo ya kuzaliwa.
Tangu kulazwa kwa Mandela huko Pretoria, Rais Zuma amekuwa akiwahimiza wananchi wake wajiandae kusherehekea miaka 95 ya Mandela akiwatia moyo wale waliokuwa na wasiwasi kwamba Madiba asingeweza kuifikia leo kutokana na matatizo ya kiafya.
Siku ya Mandela huadhimishwa kuenzi kazi za kiongozi huyo alizozifanya kwa miaka 67 akiutumikia umma wa wananchi wa Afrika Kusini, zikiwamo vita dhidi ya ubaguzi wa rangi na hatimaye kuwa Rais wa kwanza mzalendo kwa miaka mitano, kisha kustaafu.
Pia ‘Mandela Day’ hutumika kukumbuka kampeni yake dhidi ya ubaguzi wa rangi na utetezi wa haki za binadamu maarufu kwa jina la “46664”, ambayo ni namba ya utambulisho aliyoitumia alipokuwa mfungwa katika Gereza la Visiwa vya Robben.
Dakika 67 za Mandela
Kwa maana ya Siku ya Mandela ambayo pia imeidhinishwa na kutambuliwa na Umoja wa Mataifa, wananchi wa Afrika Kusini wanatumia dakika 67 kufanya shughuli mbalimbali za kijamii ikiwa ni hatua ya kuenzi kile wanachokiita ‘kazi za mtu aliyejitoa maisha yake kwa ajili ya kupigania haki na utu’.
Dakika hizo 67 zinawakilisha idadi kama hiyo ya miaka ambayo Mandela alitumika, hivyo Waafrika Kusini watakuwa wakitoa msaada na huduma kwa jamii iwe ni kwa watoto yatima au watu wengine ambao ni wahitaji katika jamii.
Kituo cha Kumbukumbu ya Mandela kimewataka wananchi kuungana na kuonyesha ushirikiano wao kwa Mandela kwa kutumia dakika 67 za muda wao kuzisaidia jamii zao ili kumuenzi kiongozi huyo ambaye ni alama ya dunia.

Monday, July 15, 2013

JESHI LA KENYA LA KANUSHA UPORAJI MAKAA YA MAWE SOMALIA

Jeshi la Kenya limekanusha madai kuwa limekuwa likipora raslimali ya Somalia kwa kuhusika na uuzaji wa makaa katika mji wa bandari wa Kismayo.
Ripoti ya wachunguzi wa Umoja wa Mataifa inaishtumu jeshi la Kenya kwa kuuza makaa nje ya Somalia kinyume na sheria katika Bandari hiyo ya Kisimayo.
Kamati kuu ya usalama ya Umoja wa Mataifa ilikuwa imepiga marufuku uuzaji wa bidhaa zote zinazoshukiwa kuwa vitega uchumi wa kundi la wapiganaji wa kiislamu la al Shabab kuanzia mwezi februari mwaka uliopita, ili kuzuia wapiganaji hao wa waasi kupata fedha za kufadhili shuguhuli zao ikiwa ni pamoja na ununuzi wa silaha na kuwalipa mishahara wapiganaji wake.
Bandari hiyo ya Kismayo iko chini ya jeshi la umoja wa Afrika kwa pamoja na serikali ya Somalia tangu ilipokombolewa kutoka kwa wapiganaji wa Kiislamu wa Al Shabaab.
Jeshi la Kenya kwa sasa ndilo linalohudumu mjini Kismayo na katika maeneo kadhaa ya Kati na Kusini mwa Somalia.

UCHUNGUZI MAUAJI YA WANAJESHI



Msemaji Mkuu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Kanali Kapambala Mgawe akizungumza na waandishi wa habari  kuhusu askari wa kulinda amani wa Tanzania waliouawa Dafur, Sudan.Kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Kulinda Amani, Meja Sadala Kapungu. 
0
Share
Dar es Salaam. Wakati Rais Jakaya Kikwete na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Ban K-Moon, wamelaani mauaji ya wanajeshi wa Tanzania Jimbo la Darfur, Sudan,  Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) limeunda timu ya kuchunguza tukio hilo.
Wapiganaji saba kati ya 36 wa Tanzania waliokuwa kwenye Jeshi la Kulinda Amani la Umoja wa Mataifa, (Unamid), waliuawa  Jumamosi na wengine 19 kujeruhiwa.
Mashambulizi hayo yalitekelezwa karibu na kambi ya Manawashi eneo la Khor Abeche, mji wa Darfur Jimbo la Nyala.
Msemaji wa JWTZ, Kanali Kapambala Mgawe, alisema Dar es Salaam jana kuwa timu ya wataalamu itakwenda Darfur kuchunguza tukio hilo.
Tukio hilo limekuwa la kushtua, kwani miaka mitano ya majeshi ya kulinda amani kuwa huko haijawahi kutokea mauaji makubwa kiasi kile.
 Kanali Mgawe alisema wanawasiliana na UN kufanya taratibu za kurudisha nyumbani miili ya wapiganaji hao.
Taarifa ya Unamid
Taarifa ya iliyotolewa jana na Msemaji wa Unamid, Christopher Cycmanick,   ilisema wanajeshi hao waliuawa walipokuwa kwenye doria ya kawaida.
Cycmanick alisema walinzi hao wa amani walishambuliwa kwa bunduki na silaha nzito za kivita umbali wa kilomita 25 kutoka katika kambi yao.
JK atuma salamu za pole
Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Rais Kikwete ameeleza kushtushwa na tukio la kushambuliwa na kuuawa wapiganaji wa JWTZ Mji wa Darfur, Sudan.
Taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano, Ikulu, ilisema Rais Kikwete ametuma salamu za rambirambi kwa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Davis Mwamunyange, familia na wapiganaji wote.

CHADEMA KIDEDEA



Askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU)wakiimarisha ulinzi kwenye Ofisi ya Mtendaji wa Kata ya Kaloleni wakati wa uchaguzi mdogo wa udiwani wa kata hiyo uliofanyika jana.Picha na Filbert Rweyemamu. 

Posted  Jumatatu,Julai15  2013  
Kwa ufupi
  • Yaibuka na ushindi wa kishindo katika kata zote nne za Arusha Mjini, wapiga kura  wengi washindwa kujitokeza
Arusha. Chadema kimethibitisha umwamba wake katika siasa za Jimbo la Arusha Mjini, baada ya kutetea kwa kishindo kata zake nne kwenye uchaguzi mdogo wa udiwani uliofanyika jana.
Katika uchaguzi huo uliokuwa unasubiriwa kwa hamu na ambao ulichukuliwa kama kipimo cha siasa za Arusha ambazo zimekuwa na mvutano mkubwa, Chadema kiliongoza katikia vituo vyote 136 vya kupigia kura Kata za Elerai, Kaloleni, Kimandolu na Themi.
Kata hizo zilikuwa wazi tangu mwaka 2011 baada ya Chadema kuwatimua wanachama wake waliokuwa madiwani Estomih Mallah(Kimandolu), John Bayo (Elerai), Reuben Ngowi (Themi) na Charles Mpanda (Kaloleni).
Matokeo
Katika matokeo yaliyotangazwa na Msimamizi wa Uchaguzi Kata ya Elerai, Obedi Meng’oriki mshindi alikuwa Jeremiah Mpinga wa Chadema aliyepata kura 2,047 dhidi ya 1,471 za Emmanuel Laizer wa CCM. Katika Kata hiyo kulikuwa na wagombea wengine ambao ni John Bayo (CUF; kura 302), Seif Shimba (CCK; kura 3) na Boisafi Shirima (TLP;1).
Katika Kata ya Themi, Kinabo Edmund wa Chadema aliibuka na ushindi baada ya kupata kura kupata kura 674. Msimamizi wa Uchaguzi Kata hiyo, Ezeka Mboya alisema Kinabo alifuatiwa na Victor Mkolwe aliyepata kura 326 na Lobora Ndarpoi wa CUF alipata kura 307.
Kata ya Kaloleni, Msimamizi wa Uchaguzi, Anna Ledisa alimtangaza Kessi Lewi wa Chadema kuwa mshindi kwa kura 1,470 dhidi ya Emmanuel Mliari wa CCM aliyepata kura 330 na Abbas Mkindi wa CUF aliyepata kura 275 na Ngilishi Pauli wa Demokrasia Makini aliyeambulia kura mbili.
Kata ya Kimandolu, Msimamizi wa Uchaguzi, Suleiman Kilingo alimtangaza Mchungaji Rayson Ngowi wa Chadema kuwa mshindi kwa kura 2,761 na kumshinda Edna Saul wa CCM aliyepata kura 1,163. Kwa matokeo hayo, Chadema sasa kimefikisha madiwani 12 wakati CCM kimebakiwa na kumi na moja na TLP kina wawili.
Ushindi huo wa Chadema una athari kwa nafasi ya Meya wa Jiji la Arusha, Gaudence Lyimo kwani CCM kina wajumbe 14 tu kwenye Baraza la Madiwani, TLP wawili wakati Chadema sasa kimefikisha 15. Wabunge wa majimbo na wale wa viti maalumu pia ni madiwani.
Aidha, Chadema kina nafasi ya kuongeza kiti kingine cha udiwani kwani Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kinatarajiwa kuitisha uchaguzi mdogo Kata ya Sombetini.
Mkurugenzi wa NEC, Julius Malaba alimwambia mwandishi wetu kuwa tume yake inatarajia kuitisha uchaguzi mdogo hivi karibuni baada ya kata hiyo kutangazwa wazi na Ofisi ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tamisemi.
Malaba alisema uchaguzi huo utaitishwa baada ya aliyekuwa Diwani wake, Alphonce Mawazo kujitoa CCM na kujiunga na Chadema hali inayokifanya chama tawala kuwa katika wakati mgumu kukitetea kiti hicho.

Sunday, July 14, 2013

Mbowe adai polisi walivamia usiku makazi yake D’Salaam

Dar es Salaam. Polisi kadhaa wanadaiwa kuvamia nyumbani kwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, kwa lengo la kumkamata.
Habari zilizopatikana na kuthibitishwa na Mbowe mwenyewe zinaeleza kuwa askari hao waliokuwa na silaha walivamia nyumba hiyo iliyopo eneo la Mikocheni, jijini Dar es Salaam usiku wa kuamkia jana wakiwa na silaha.
Mbowe alisema hata hivyo walikwama kumkamata, kwa sababu alikuwa nje ya Dar es Salaam kwa shughuli za chama.
Hata hivyo, mwenyekiti huyo alikataa kuzungumzia zaidi suala hilo akieleza kuwa anayeweza kulizungumzia zaidi ni Ofisa Habari wa chama hicho, Tumaini Makene.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni, Camillius Wambura alipoulizwa alisema kuwa hana taarifa za polisi kumtafuta Mbowe.
“Sina taarifa polisi wangu kumtafuta Mbowe,” alisema Wambura.
Lakini Ofisa Habari wa Chadema Tumaini Makene aliliambia Mwananchi Jumapili jana kuwa askari hao walifika nyumbani kwa Mbowe saa 7:16 usiku, wakidai kuwa na hati ya kumkamata Mbowe kutokana na makosa ambayo hata hivyo hawakuyabainisha.
“Ni kweli askari walifika nyumbani kwa Mwenyekiti wakidai walikuwa wakihitaji kumkamata. Kinachotushangaza ni kwamba mtu ambaye anafahamika na wanajua ni mbunge na kiongozi wa chama, lakini wanakwenda kumkamata kama jambazi, usiku wa manane,” alisema Makene.
Alisema kuwa polisi hao walifika nyumbani kwa Mbowe na kukutana na walinzi katika nyumba hiyo, waliowaeleza kuwa mwenyekiti huyo wa Chadema alikuwa safarini.
Makene hakuwataja majina walinzi waliokutwa , lakini nalisisitiza kwamba polisi hao waliacha namba za simu kwa walinzi hao, wakitoa maelezo kuwa pindi Mbowe atakaporejea wamwarifu na kuwapigia polisi kwa kuwa alikuwa akihitajika kituoni.
Ofisa huyo alieleza kuwa wakati wa tukio hilo Mbowe hakuwapo nyumbani na alikuwa safarini mkoani Kilimanjaro, kuhudhuria vikao vya Halmashauri ya Hai.
Makene alisema wanashangazwa na vitendo vya Polisi kusaka viongozi wao usiku wa manane kama majambazi sugu, wakati wakifahamika ni wabunge.

UCHAGUZI ARUSHA VURUGU ZATAWALA

Masanduku ya kuhesabia kura uchaguzi mdogo wa madiwani Arusha 
Kwa ufupi
Mbali ya NEC kupiga marufuku viongozi hao wa kisiasa kukaribia vituo hivyo, uchaguzi huo umekumbwa na matukio kadhaa likiwamo la Mbunge wa Jimbo la Arusha, Godbless Lema pamoja na Mwenyekiti wa Baraza la Vijana la Taifa Chadema(Bavicha), John Heche, kunusurika kuswekwa rumande jana
0
Shar
Arusha. Uchaguzi mdogo katika kata nne za Jiji la Arusha unafanyika leo, huku Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), ikiwapiga marufuku Mkuu wa Mkoa, Magessa Mulongo na Mkuu wa Wilaya ya Arusha, John Mongella kuingia kwenye vituo vya kupigia kura, wala kujihusisha kwa namna yoyote na zoezi la upigaji kura ikisema siyo jukumu lao kisheria.
Mbali ya NEC kupiga marufuku viongozi hao wa kisiasa kukaribia vituo hivyo, uchaguzi huo umekumbwa na matukio kadhaa likiwamo la Mbunge wa Jimbo la Arusha, Godbless Lema pamoja na Mwenyekiti wa Baraza la Vijana la Taifa Chadema(Bavicha), John Heche, kunusurika kuswekwa rumande jana.
“RC na DC hawana haki wala mamlaka ya kujihusisha kwenye zoezi na shughuli za upigaji kura. Mwenye dhamana, wajibu na haki ya shughuli zote za upigaji kura ni Mkurugenzi wa Jiji ambaye ni mwakilishi wa NEC pamoja na maofisa wengine wanaotambuliwa kisheria,” alisema Mwenyekiti wa NEC Jaji Damian Lubuva jana.
Lema na Heche walinusurika kuswekwa rumande baada ya kufika Kituo Kikuu cha Polisi jijini Arusha, wakishinikiza jeshi hilo, kukamata magari matatu waliyodai kuwa ni ya Chama Cha Mapinduzi(CCM) na kubadilishwa namba yakihofiwa kwamba huenda yakatumika kuvuruga uchaguzi wa leo.
Tukio hilo la aina yake, lilitokea jana asubuhi baada ya viongozi hao, kufika polisi na kutoa taarifa hiyo, wakieleza kuwa lakini waliambiwa waondoke kwa kuwa gari kubadili namba siyo kosa ambapo pia walitakiwa kumtaja aliyewaeleza kama magari hayo yatatumika kufanya uhalifu.
Aidha, viongozi wa vyama vyote vya siasa ambao sio mawakala wala wagombea, wamepigwa marufuku kuingia kwenye vituo vya kupigia kura, wala kujihusisha kwa namna yoyote na zoezi la upigaji kura badala yake wakiwa ni wakazi wa kata husika kupiga kura na kuondoka maeneo hayo.
Mwenyekiti wa NEC, alitoa tamko la kuzuia viongozi hao jana alipozungumza na waandishi wa habari kuelezea mipango na mikakati ya tume yake katika kufanikisha zoezi hilo linalofanyika baada ya kuahirishwa mara mbili.
Mbele ya makamu wake Jaji Mkuu mstaafu wa Zanzibar, Jaji Hamid Mohamoud Hamid, Jaji Lubuva alitaja orodha ya watu 12 wenye haki kisheria kuingia kwenye vituo vya kupigia kura na kujihusisha na zoezi la upigaji, kuhesabu, kujumlisha kura kuwa ni msimamizi wa kituo, msimamizi msaidizi wa kituo, mawakala wa vyama na wapiga kura.
Wengine ni Mkurugenzi wa Uchaguzi, mgombea, mjumbe wa NEC, Ofisa wa NEC, Mratibu wa NEC mkoa, askari polisi au mtu yeyote anayehusika na usalama katika kituo cha kupiga kura, mtu anayemsaidia mpigakura asiyejiweza na mwangalizi wa uchaguzi aliyeidhinishwa na NEC kimaandishi na katika utaratibu uliowekwa.
Uchaguzi huo unafanyika leo baada ya kuahirishwa Juni 16, mwaka huu, baada ya bomu la kutupa kwa mkono kulipuka kwenye mkutano wa Chadema wa kufunga kampeni kwenye Viwanja vya Soweto, Arusha.
Agizo la kupiga marufuku kujihusisha na Uchaguzi Mkuu wa Mkoa(Mulongo) na Mkuu wa Wilaya(Mongella) ambao ni makada na wajumbe wa Kamati za Siasa na Halmashauri za Mkoa na Wilaya za CCM, limekuja wakati kukiwa na tuhuma kutoka kwa vyama vya upinzani, hasa Chadema kuwa wanatumia nyadhifa zao kukibeba chama tawala.
Akizungumzia kunusurika kuwekwa rumande, Heche alisema kutokana na majibu ya polisi wao wakiomba wapewe hata fursa ya kuandika maelezo kuhusu tukio hilo au wapewe polisi kwenda kuzikamata gari hizo, lakini waligomewa, ndipo likatolewa agizo la kukamatwa kuwekwa rumande kwa Lema.

WANAJESHI SABA WA TANZANIA WAUWAWA

Dar es Salaam. Wanajeshi saba wa Tanzania, ambao ni miongoni mwa kikosi cha Umoja wa Mataifa, cha kulinda amani katika jimbo la Darfur nchini Sudan, wanadaiwa kuwa wameuawa.
Taarifa zilizolifikia gazeti hili jana zilisema kwamba wanajeshi hao wa Tanzania, wamekufa kutokana na mashambulizi yaliyofanywa na waasi wanaopigana na Serikali.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, miili yao wanajeshi hao bado ipo nchini Sudan ikisubiri taratibu za kusafirishwa kuletwa nchini.
Hii ni mara ya kwanza kuripotiwa kwa idadi kubwa ya wanajeshi wa Tanzania wanaolinda amani katika nchi mbalimbali kufa kwa wakati mmoja.
Agosti mwaka jana wanajeshi watatu wa Tanzania huko Darfur waliripotiwa kuuawa kwenye tukio kama hilo.
Msemaji wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) , Kanali Kapambala Mgawe alipoulizwa kwa njia ya simu kuhusu vifo vya wanajeshi wa Tanzania huko Darfur, alisema kuwa naye amesikia, lakini hana taarifa rasmi kwa mujibu wa taratibu za kiofisi.
Hii ni mara ya pili kwa wanajeshi wa Tanzania kuuawa katika Jimbo la Darfur, ambapo Agosti mwaka jana, Kanali Mgawe alinukuliwa na vyombo vya habari akithibitisha kutokea kwa vifo vya askari watatu ambao gari lao lilizolewa na maji walipokuwa wakivuka mto uliokuwa umefurika maji.
Kanali Mgawe aliwataja askari hao kuwa ni Sajini Julius Chacha, Sajini Anthony Daniel na Koplo Yusuph Said na kwamba askari wengine walinusurika baada ya kuogolea.
Tanzania ina askari 850 kwenye kikosi cha Umoja wa Mataifa cha Kulinda Amani jimbo la Darfur, ambao ni sehemu ya askari 1,081 wa kulinda amani katika jimbo la Darfur.
Wanajeshi hao wa Tanzania wametawanywa kwenye miji ya Khor Abeche na Muhajeria kusini mwa Darfur.
Aprili mwaka huu Tanzania ilipeleka wanajeshi wa kulinda amani katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), kupambana na kikundi cha waasi wa nchi hiyo M23 kinachopigana kuiangusha serikali ya DRC.
Majeshi ya Tanzania yalipelekwa kulinda amani chini ya Umoja wa Mataifa. Tanzania inaungana na nchi za Afrika Kusini na Malawi kukamilisha kikosi cha wanajeshi 3,000. Tanzania imepeleka wanajeshi 850.

MOTO WASABABISHA KUFUNGWA UWANJA WA NDEGE KWA MUDA

Ndege ya aina ya Boeing 787 inayomilikiwa na Shirika la ndege la Ethiopia katika uwanja wa Heathrow
Shughuli katika uwanja wa ndege wa Heathrow zimekwama kwa muda baada ya ndege moja ya shirika la ndege la Ethiopia aina ya Boeing 787 Dreamliner kushika moto.
Safari zote za ndege katika uwanja huo zilisitishwa kuanzia saa kumi na nusu.
Kwa mujibu wa msemaji wa mamlaka ya uwanja wa ndege wa Heathrow, hakuna abiria aliyekuwa ndani ya ndege hiyo wakati wa tukio hilo.
Mapema mwaka huu ndege hamsini aina ya Dreamliners, zilisimamishwa kufanya kazi kutokana na matatizo ya mtambo wa Battery.
Mwezi April, ndege moja ya shirika la ndege la Ethiopia, ambalo limesemekana kuwa ndilo lililopata matatizo katika uwanja wa Heathrow, ilisafiri kutoka Adis Ababa hadi Nairobi kwa mara ya kwanza tangu mwezi Januari.
Picha zilizochapishwa kwenye mtandao wa Kijamii wa Twitter, zimeonyesha ndege moja katika uwanja huo ikiwa imezingirwa na magari ya kuzima moto.
Wafanyakazi wa idara ya kuzima moto ya baraza la mji wa London wamesema kuwa walikuwa tayari kushirikiana na maafisa wa kitengo cha kupambana na mikasa ya moto katika uwanja huo.

MAREKANI NA UJERUMANI WATAKA MURSI AWE HURU

Matukio ya Afrika

Marekani, Ujerumani zataka Mursi aachiliwe

Kundi la Udugu wa Kiislamu limeitisha maandamano makubwa ya umma nchini Misri siku ya Jumatatu huku Marekani ikiungana na Ujerumani kutaka kuachiliwa huru kwa rais aliyepinduliwa na jeshi, Mohamed Mursi.
Wito wa Udugu wa Kiislamu umetolewa masaa kadhaa baada ya maelfu ya wafuasi wa Mursi kuingia mitaani kwenye maandamano ya amani ya kudai kuachiliwa kwa kiongozi wao mjini Cairo.
"Jumatatu ijayo, Mungu akipenda, umma mkubwa utakusanyika kwenye viwanja vyote vya Misri dhidi ya mapinduzi haya ya kijeshi. Misri huamua kupitia kura na maandamano maandamano ya amani. Hakuna yeyote, kundi lolote au taasisi ya kijeshi itakayolazimisha maamuzi yake kwa watu wa Misri," amesema Essam El-Erian wa chama cha Uhuru na Haki, ambacho ni tawi la kisiasa la Udugu wa Kiislamu.
Kundi la Udugu wa Kiislamu limekataa aina yoyote ya mazungumzo ya kisiasa tangu wakati huo, likishikilia kwamba ni lazima Mursi arejeshwe madarakani.
Marekani, Ujerumani zataka Mursi aachiliwe
Maandamano ya kumuunga mkono Mohamed Mursi mjini Cairo siku ya tarehe 12 Julai 2013. Maandamano ya kumuunga mkono Mohamed Mursi mjini Cairo siku ya tarehe 12 Julai 2013.
Siku ya Ijumaa, Marekani ilitoa wito kwa jeshi la Misri kumuachia Rais Mohamed Mursi, ikisema inaungana na Ujerumani ambayo ilitangulia kutoa wito kama huo.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje, Jen Psaki, alisema nchi yake inakubaliana na Ujerumani katika hilo na kwamba ilitoa ombi hilo hadharani. Licha ya serikali ya mpito kusema kwamba Mursi yuko salama, lakini hajaonekana hadharani tangu alipopinduliwa na jeshi tarehe 3 Julai.
Psaki alisema Marekani inataka kuondolewa kwa usiri juu ya taarifa za wapi alipo Mursi, ambapo Ujerumani ilipendekeza kwamba taasisi inayoaminika, kama vile Shirika la Msalaba Mwekundu, ipewe fursa ya kumuona na kumuhudumia Mursi.
Maandamano yapamba moto
Maandamano ya kumuunga mkono Mohamed Mursi mjini Cairo siku ya tarehe 12 Julai 2013. Maandamano ya kumuunga mkono Mohamed Mursi mjini Cairo siku ya tarehe 12 Julai 2013.
Maandamano tafauti ya kumuunga mkono na kumpinga Mursi yalifanyika mjini Cairo siku ya Ijumaa (tarehe 12 Julai), kwa njia ya amani licha ya hofu za awali kwamba yangelikumbwa na machafuko.
Magharibi ilipoingia, maelfu ya wafuasi wa Mursi kwenye mitaa kadhaa ya Cairo waliswali na kukata swaumu zao, ikiwa ni Ijumaa ya kwanza tangu kuanza mwezi mtukufu wa Ramadhani, ambapo katika uwanja maarufu wa Tahriri na nje ya kasri ya rais ya Ittihadiyya, mamia ya waandamanaji wanaompinga Mursi walifutari pamoja.
Wafuasi wa Mursi wamekuwa wakiandamana pia nje ya msikiti wa Rabaa al-Adawiya katika mji wa Nasr, ambako wakiwa wamebeba Qur'an na bendera za Misri, wanasikikana wakipiga mayowe ya kuyalaani mapinduzi ya kijeshi yaliyomuondoa rais wa kwanza kuchaguliwa kidemokrasia.
"Tutaendelea kupambana," kiongozi wa ngazi za juu wa Udugu wa Kiislamu, Safwat Hegazi aliuambia umma siku ya Ijumaa. "Tutakaa hapa kwa mwezi mmoja au miwili, au hata mwaka mmoja au miwli. Hatutaondoka hadi rais wetu, Mohamed Mursi, arudi."
Hayo yanatokea katika wakati ambapo waziri mkuu wa serikali ya mpito, Hazem el-Beblawi, anatarajiwa kuliapisha baraza jipya la mawaziri wiki ijayo.
Baraza hilo lina jukumu la kuutekeleza mpango wa jeshi kuelekea utawala wa kiraia, baada ya jeshi kumpindua rais wa kwanza kuchaguliwa kidemokrasia hapo tarehe 3 Julai

KUELEKEA UCHAGUYI MKUU ZIMBABWE

Matukio ya Afrika

Mugabe, Tsvangirai uwanjani

Mahasimu wa kisiasa nchini Zimbabwe, Rais Robert Mugabe na Waziri Mkuu Morgan Tsvangirai wamenadi sera zao kwa malengo ya kulikwamua taifa hilo kiuchumi, ikiwa ni jitihada za kuwavutia wapiga kura kabla ya Machi 31.
Kwa mujibu wa tathmi ya shirika la habari la Ufaransa AFP mahasimu hao "walirindima", mwishoni jumamosi ikiwa zimebaki wiki si zaidi ya tatu kufanyika kwa uchaguzi mkuu wa taifa hilo, unaotarajiwa kufikisha kikomo serikali yao ya mizengwe iliyolazimishwa kuundwa kutokana na uchaguzi wenye vurugu wa 2008.
Akizungumza katika kampeni yake katika taifa hilo lenye utajiri mkubwa wa madini ya almas kwa upande wa mashariki, Tschangirai alisema " Chaguo ni rahisi sana, ni kati ya serikali iliyoshindwa kwa zaidi ya miaka 33 na ahadi mpya ambazo ziko wazi kabisa" Kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 61 alizungumza katika mji wa Mutare akimtolea mfano rais Mugabe kuwa mwenye kutaka kuhodhi madaraka.
Mugabe na sera za uzawa
Supporters cheer Zimbabwean President Robert Mugabe as he arrives to launch his ruling ZANU PF party's election manifesto in the capital Harare July 5, 2013. Zimbabwe's Constitutional Court rejected a series of government appeals on Thursday to delay a July 31 general election in order to allow more time for reform of the security forces and state media. REUTERS/Philimon Bulawayo (ZIMBABWE - Tags: POLITICS ELECTIONS) Wafuasi wa Robert Mugabe
Mugabe mwenye umri wa miaka 89, akiwa amevalia kanzu nyeupe huku ameshika biblia mkononi alijitokeza mbele ya maelfu ya wafuasi wake waliokusanyika katika eneo la kanisa moja huko mjini Marange, umbali wa kilometa 200, mashariki mwa mji mkuu Harare. Akinukuliwa na AFP kiongozi huyo mkongwe barani Afrika alisema"Tulifanya makosa 2008 kumchagua mtu ambae anapenda Wazungu. Kumpigia kura mtu ambae anataka kuwarejesha wazungu na ambae anafikiri haiwezekani kuwepo kwa maendeleo nchini Zimbabwe bila kuhusishwa watu hao" Alisema rais Mugabe.
Katika kunadi sera zake kiongozi huyo mkongwe alilenga masuala ya uzawa, au sera za uzawa na kuwawezesha watu weusi akisema kwamba Zimbabwe lazima imiliki sehemu kubwa ya rasilimimali yake. Kwa upande wake Tsvangirai ameahidi kurekebisha uchumi, kufufua viwanda na kuvutia uwekezaji kwa lengo la kupanua wigo wa ajira kwa vijana nchini humo.
Almas kwa Wazimbabwe wote
Zimbabwe opposition Movement For Democratic Change (MDC) leader Morgan Tsvangirai speaks at the launch of his party's election campaign in Marondera, about 70 km (43 miles) east of Harare, July 7, 2013. Tsvangirai, launching his third campaign to unseat veteran President Robert Mugabe, said nothing had been achieved to ensure a fairer vote but even God now wanted Mugabe to go. REUTERS/Philimon Bulawayo (ZIMBABWE - Tags: POLITICS ELECTIONS) Mgombea urais Zimbabwe Morgan Tsvangirai
Akizungumza mbele ya maelfu ya wafuasi waliovaa fulana nyekundu zenye picha yake. Tsvangirai ameahidi kufanikisha uwazi katika uchimbaji wa madini ya almas. Nikimunukuu kiongozi huyo wa upinzani hapa alisema " Wapi zinapokwenda fedha za almas? Tunafahamu tukipata fedha zote kutoka katika madini hayo tunaweza kuunda ajira mpya laki moja. Alisema katika mkutano wake wa kampeni uliyofanyika katika uwanja wa Mutare, uliyopo kilometa 250 mashariki mwa Zimbabwe.
Aliongeza kusema kama mapato yote kutoka katika madini hayo yangefika moja kwa moja katika mikono ya serikali wangaliweza kulia walimu na wanajeshi na sio kama ilivyo sasa ambapo mapato hayo yanawanufaisha watu wachache. Kama atapewa ridhaa ya Wazimbabwe kuongoza taifa hilo Tsvangirai ameahidi kupitia upya mikataba yote katika sekta ya madini kwa kuwa ya sasa inatoa mianya ya kuendelea kwa vitendo vya rushwa.
Aidha katika kampeni yake rais Robert Mugabe amepinga ndoa za jinsia moja kuwa zinakwenda kinyume na utamaduni wa Afrika na kuikosoa vikali kauli ya rais Obama barani wakati alipozulu Afrika kuhimiza waafrika kuheshimu haki za mashoga. Mugabe alisisitza kauli yake hiyo kwa kusema ndoa ni ya mwanamke na mwanaume ambapo matunda yake ni kuzaliwa watoto.
Katika uchaguzi uliyopita Zimbabwe iligubikwa na visa vya umwagikaji damu. Tsvangirai alijiondoa katika kinyanganyiro hicho pamoja na cha mwaka 2008 pamoja na kuibuka na ushindi katika duru ya kwanza. Uchaguzi wa mwezi huu unatajwa kuwa wenye kuweza kuifikisha serikali ya mseto nchini humo ambayo imesababisha kudidimia kwa uchumi.

MAANDAMANO TENA MISRI

Wafuasi wa rais wa zamani wa Misri Mohamed Morsi
Wafuasi wa rais wa Misri aliyeondolewa madarakani Mohammed Morsi wamefanya maandamano makubwa mjini Cairo, huku waumini wa dini ya Kiislamu wakiadhimsiha Ijumaa ya kwanza tangu kuanza kwa mwezi mtukufu wa Ramadan.
Wafuasi wa kiongozi huyo wa vugu vugu la Muslim Brotherhood walijikusanya Mashariki mwa mji huo, kushinikiza utawala wa kijeshi kumrejesha madarakani kiongozi wao.
Wapinzani wa rais huyo wa zamani ambao waliandamana hadi rais huyo akaondolewa madarakani na jeshi watakusanyika katika medani ya Tahrir.
Watu kadhaa wameuawa kwenye ghasia zilizotokea tangu Morsi alipoondolewa.
Mwandishi wa BBC mjini Cairo, Jim Muir anasema vuguvugu la Muslim Brotherhood huenda liliwatenga raia wengi wakati wa utawala wa Morsi, lakini bado raia wengi wa nchi hiyo hawataki jeshi kuingilia masuala ya siasa.

Marekani kutuma ndege za kivita Misri

Siku ya Alhamisi serikali ya Marekani, ilitoa wito kwa utawala mpya wa Misri, kusitisha harakati zake za kuwakamata wanachama wa vuguvugu la Muslim Brotherhood na kuonya dhidi ya kulenga kundi lolote.
Wanajeshi wakishika doria mjini Cairo
Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon vile vile ameonya utawala huo wa Misri kutotenga chama chochote cha kisiasa katika harakati za kutatua mzozo wa kisiasa unaokumba taifa hilo.
Hata hivyo msemaji wa Ikulu ya White House, Jay Carney amesema, utawala wa Washington hauamini kuwa ni lazima isitishe misaada yake ya Misri.
Marekani inatarajiwa kupeleka ndege nne za kivita aina ya F-16 nchini Misri, lakini haijathibitisha kuwa msaada huo utatolewa lini.
Serikali ya Marekani imesema, inachunguza ikiwa aumuzi huo wa jeshi la Misri kumuondoa madarakani rais Morsi ni mapinduzi ya Kijeshi kwa kuwa sheria za Marekani inazuia serikali kutoa misaada kwa nchi yoyote ambayo kiongozi aliyechaguliwa kwa njia ya kidemokrasia ataondolewa kupitia mapinduzi.
Wafuasi wa rais Morsi wamekuwa wakiandamana wiki nzima karibu na kambi ya kijeshi iliyoko Mashariki mwa mji mkuu wa Cairo, ambako wanaamini kuwa kiongozi wao anazuiliwa na maafisa wa kijeshi tangu alipoondolewa madarakani.

Monday, July 8, 2013

MACHINGA MSIDANGANJIKE


Askari Polisi na Mgambo wa Jiji wakiimarisha ulinzi katika eneo lamanzese jijini Dar es salaam jana, baada ya kutokea vurugu kati ya mgambo na Wamachinga zilizosababisha barabara ya Morogoro kufungwa kwa muda kwa saa tatu. 

Dar es Salaam. Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Jordan Rugimbana amewataka wafanyabiashara ndogondogo (wamachinga) kutodanganywa  na wanasiasa kwa lolote kwani mpango wa kuwaondoa maeneo wasiyotakiwa ni wa lazima. “Leo tunaendelea mitaa ya Manzese, Ubungo na hata Mwenge kwani ni lazima waondoke ili kazi za umma zifanyike’’ alisema.
Kauli ya Rugimbana imekuja ikiwa ni siku moja baada ya kutokea vurugu za wafanyabiashara na polisi wa kutuliza ghasia na mgambo wa jiji waliokuwa wakiwataka kuondoka katika eneo hilo ili kutoa nafasi ya mradi wa ujenzi wa barabara wa mabasi yaendayo kasi (BRT) eneo hilo.
Rugimbana alisema baadhi ya wanasiasa wanatumia majukwaa yao vibaya kwa kuwadanganya wafanyabiashara hao hilo zoezi la kuhamishwa eneo la Manzese ilikuwa ni la muda mfupi kwa ajili ya ujio wa Rais Barack Obama. Akizungumza na Mwananchi kwa simu jana, Rugimbana alisema zoezi la kuwahamisha wamachinga hao ni la kisheria kwa sababu  lazima waondoke ili kumpisha mkandarasi aendelee na ujenzi wa barabara hiyo.
“Tuna mgongano na baadhi ya wanasiasa ndio wanaoturudisha nyuma wanawapotosha hawa wamachinga, sisi tunafuata sheria sio siasa lazima waondoke ili mkandarasi aendelee kufanya kazi eneo lile,” alisema Rugimbana.
Rugimbana  alisema  zoezi hilo ni endelevu hivyo yeyote atakayeenda kinyume na agizo hilo atachukuliwa hatua za kisheria hivyo wametakiwa kuondoka eneo hilo.
Alisema wafanyabiashara hao kama wana matatizo wanatakiwa wamuone mkuu huyo, Meya wa manispaa hiyo ili waweze kukaa pamoja na kutatua matatizo yao.
“Hili zoezi ni endelevu na leo hii oparesheni itaendelea maeneo yote ambayo hayaruhusiwi kama Ubungo, Manzese na Mwenge, kama eneo la Mwenge tumewaondoa wafanyabiashara na vibanda vyao vimebomolewa  ili kupisha upanuzi wa barabara,”

HATIMA YA MAKAMANDA WA CHADEMA KUJULIKANA TABORA

Dar es Salaam. Hatima ya makada watano wa Chadema, wanaokabiliwa na kesi ya ugaidi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Tabora, inatarajiwa kujulikana leo, wakati mahakama hiyo itakapotoa uamuzi kuhusiana na kesi hiyopamoja na mambo mengine, uhalali wa mashtaka yanayowakabili.
Makada hao wa Chadema, Henry John Kilewo, ambaye ni Katibu wa Chadema Wilaya ya Kinondoni,  Evodius Justinian, Oscar Kaijage,  Rajabu Daniel, Seif Magesa Kabuta, walipandishwa kizimbani mahakamani hapo na kusomewa mashtaka mawili, moja la ugaidi na lingine la jinai.
Katika shtaka la kwanza wanashtakiwa chini ya Sheria ya Kuzuia Ugaidi, wakidaiwa kumteka kwa nia ya ugaidi Mussa Tesha huko Igunga, Tabora,  na la pili wanashtakiwa chini ya Sheria ya Kanuni za Adhabu wakidaiwa kumdhuru Tesha kwa kumwagia tindikali.
Walidaiwa kutenda makosa hayo mwaka 2011, wakati wa kampeni za uchaguzi mdogo wa Jimbo la Igunga.Baada ya kusomewa mashtaka hayo, mawakili wao, Peter Kibatala na Profesa Abdallah Safari walipambana kuwanusuru na mashtaka hayo.
Mawakili hao walihoji uhalali wa mashtaka hayo,wakidai kuwa hakuna vigezo vya kutosha kuonyesha kuwa kuna ugaidi, huku pia wakihoji utaratibu wa kuwafungulia mashtaka katika mahakama hiyo badala ya kule walikokamatiwa.
Hivyo waliiomba Mahakama hiyo ama iwafutie mashtaka hayo au iamuru kila mshtakiwa arudishwe na kushtakiwa katika mahakama za mahali walikokamatiwa.
Upande wa mashtaka ukiongozwa na Wakili wa Serikali, Juma Masanja akisaidiana na Wakili wa Serikali, Idelfonce Mukandara, walidai mashtaka hayo ni halali.
Baada ya kusikiliza hoja za pande zote, Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Joctan Rushwera aliahirisha kesi hiyo na kupanga kutoa uamuzi leo.
Hakimu Rushwera aliamuru washtakiwa wote wapelekwe mahabusu wakisubiri uamuzi wa kesi yao leo, kwa kuwa mashtaka yanayowakabili hayana dhamana.

WAFA KWA MAANDAMANO MISRI

Takriban watu 15 wameuawa mjini Cairo kufuatia ghasia nje ya kambi ya kijeshi ambapo wafuasi wa aliyekuwa rais wa taifa hilo Mohammed Morsi wanaamini kiongozi huyo anazuiliwa.
Haya yanajiri huku ghasia zikiendelea baada ya kuondolewa mamlakani kwa aliyekuwa rais Mohammed Morsi.
Waandamanaji hao wanasema vikosi maalum viliwafyatua risasi baada ya swala ya fajir huku wengine wakishambuliwa walipokusanyika nje ya makao ambako bwana Morsi anadhaniwa kuzuiliwa wakitaka watawala kumwachilia huru.
Msemaji wa chama cha Muslim brotherhood amesema kuwa idadi ya waliofariki katika ghasia hizo imefikia 30 huku zaidi ya watu 500 wakijeruhiwa.
Lakini katika taarifa yake, jeshi la nchi hiyo limesema kuwa kundi moja la kigaidi lilikuwa likijaribu kuingia katika kambi hiyo na kumuua mwanajeshi mmoja.
Limeongezea zaidi ya watu 200 walitiwa mbaroni wakimiliki silaha kama vile visu.
Duru kutoka wizara ya afya zilisema kuwa afisaa mmoja wa jeshi aliuawa.
Bwana Morsi, aliyekuwa rais wa kwanza wa kiisilamu kuchaguliwa kidemopkrasia Misri, aling'olewa mamlakani na jeshi, siku ya Jumatano baada ya kufanyika maandamano makubwa.
Mmoja wa waandamanaji Mahmud al-Shilli, aliambia shirika la habari la AFP kuwa wanajeshi waliwarushia gesi ya kutoa machozi lakini kikundi cha wanaume waliokuwa wamevalia mavazi ya kiraia ndio waliwafyatulia risasi.
Katika taarifa iliyosomwa kwenye vyombo vya habari vya serikali, jeshi lililaumu kikundi cha watu walaiokuwa wamejihami ambao limesma ni mgaidi waliokuwa na njama ya kuvamia kambi ya jeshi.

Saturday, July 6, 2013

MISRI MISRI MISRI

Sherehe zilijaa kote Misri baada ya Morsi kuondolewa mamlakani
Jaji mkuu wa mahakama ya juu zaidi ya kikatiba ameapishwa nchini Misri kuwa rais wa muda baada ya jeshi kumng'oa mamlakani rais aliyechaguliwa na raia kwa njia ya kidemokrasia na kushinda kwa wingi wa kura, Mohammed Morsi.
Viongozi duniani wamepokea kwa tahadhari matukio yanayojiri huko Misri. Waziri wa mashauri ya kigeni wa Ujerumani, Guido Westerwelle, amewaambia waandishi kwamba anaangalia kwa umakini hatua iliyochukuliwa na jeshi la Misri.
Waziri wa mashauri ya kigeni wa Uingereza , William Hague, amesema Uingereza haiungi mkono uvamizi huo wa kijeshi lakini haina budi kuitambua hatua hiyo na kusogea mbele. Hata hivyo alikataa kulishutumu jeshi kwa kumpindua Morsi akisema ni uvamizi ulioungwa mkono na watu wengi.
Mfalme Abdalla wa Saudia ametuma ujumbe wa hongera kwa kaimu rais wa Misri akisema kwamba uteuzi wake unajiri katika wakati muhimu.
Mkuu wa jeshi Generali Abdul Fattah al-Sisi alitoa tangaza hilo kupitia televisheini Jumatano jioni, katika kile Morsi, alisema ni mapinduzi ya kijeshi.
Generali Sisi alisema kuwa Morsi,ambaye ni rais wa kwanza kuchaguliwa amekosa kutimiza mahitaji ya watu.
Ishara ya mapenzi iliyochorwa angani kwa kutumia ndege za kijeshi kuwataka wananchi kupatana
Hatua hiyo inakuja baada ya siku nyingi ya maandamano, dhidi ya rais Morsi wa chama cha Musolim Brotherhood.
Waandamanaji walimtuhumu yeye na chama chake kwa kusukuma ajenda ya kiisilamu kwa taifa hilo na kukosa kusuluhisha matatizo ya kiuchumi yanayokumba taifa hilo.
Chama cha Muslim Brotherhood kimesema kuwa bwana Morsi pamoja na washauri wake wako chini ya kifungo cha nyumbani na hawana mawasiliano ya nje.
Hapo awali mkuu wa majeshi alisema kuwa katiba ya nchi hiyo imeahirishwa na kwamba jaji mkuu wa taifa hilo atachukuwa mamlaka ya rais.
Maelfu ya waandamanaji wanaompinga bwana Morsi mjini Cairo walisherehekea kwa shangwe na vifijo kufuatia taarifa hiyo ya jeshi lakini wale wanaomuunga bwana Morsi wanasemekana kubaki kimya huku wakisubiri matukio yatakayofwata.
Rais Obama amesema kuwa ana wasiwasi mkubwa kuhusiana na matukio yaliyopo nchini Misri huku katibu mkuu wa umoja wa mataifa Banki Moon akitaka kuwe na utulivu.

Wednesday, July 3, 2013

KWELI TANZANIA KUNA AMANI YA KUDUMU?



Wasomaji wangu ni matumaini yangu muu wazima wa afya na mnaendelea vyema na majukumu mbalimbali  ya kujenga taifa na jamii zetu kiujumla.
          Watanzania tumeendelea kuishi kwa amani na furaha huku tukishuhudia ujio wa wakuu wa nchi mbalimbali kuba hapa duniani.Tumeona raisi wa China akiwasili nchini na pia raisi wa Marekani pia amefika nchini na msafara mkubwa. Wote wa hao wamepongeza utawala uliopo tanzania na amani iliyopo.Watawala wa Tanzania wamebaki wakijisifu kwamba wamedumisha utawala bora pengine kuliko nchi nyingine za Afrika.
           Ni wakati wetu watanzania kujiuliza je ni kweli kuna amani ya kudumu Tanzania? Na pia je kuna utawala bora Tanzania?.Haya maswali magumu hayaweyi kujibiwa na viongoyi walioko madarakani bali ni kwa sisi wananchi wa Tanzania kwa kutoa maoni na fikra  zetu.
       Tukianza na utawala bora,mtu akisema utawala bora ina maana ya utawala unaofuata sheria na misingi uongozi na sheria na kanuni za nchi husika.Kwa ripoti mbalimbali na matukio yanayoendelea Tanzania hatuwezi kusema kuna utawala bora nchini.Ufisadi umekua kama hulka  ya viongozi wetu kama ule wa Richmond na dowans ,rada feki naule wa majengo pacha ya BOT.Pia kuna ufisadi na ruswa iliyokisiri katika mahakama zetu,polisi na ngazi mbalimbali za uongozi hapa Tanzania.
             Licha ya ufisadi pia kuna suala la watu kutungiwa kesi za uongo,watu kufungwa muda mrefu bila kufunguliwa mashitaka na matendo mbalimbali ya kupeana ajira na huduma kwa kujuana na ucheleweshaji wa makusudi wa huduma kwa wale raia wenye kipato cha chini.Ni waji bu wa wananchi kupigana kupinga utawala mchafu usio jili matakwa ya wengi
        Kikubwa tulichonacho ni kuendelea kumshukuru mungu kwa kuendelea kutupa amani kwa zaidi ya miaka hamsini sasa.Watanzania wamekuwa wavumilivu na kuendelea kuendelea kutunza amani kwa nguvu zote.Swali linakuja na kuuliza amani hii itadumu mpaka lini?.je watanzania wataendelea kuwa wavumilivu mpaka lini?.Mikono ya sheria imewaona wanao jaribu kuvunja amani kwa nguvu zote?
               Tumeona matukio mbalimbali kama kuuwawa kwa padre kule Zanzibar,bomu kanisani Arusha,Mauaji yaliyo fanywa na polici Arusha,maandamano kule Mtwara na harakati za shehe Ponda.Je haya yote yatanusuru amani iliyopo nchini?.Je ni viashiria tosha vya kutokua na amani mwaka 2015.
          Matatizo yanayoendelea Brazil na Misri yamesababishwa na hali ngumu ya maisha na pia utawala usiojali kama wetu hapa Tanzania.Hivi ni viashiria tosha kwamba kuna kuanguka katika matatizo makubwa siku zijazo.
             Ni rai yangu kwa viongozi wetu kutafuta njia muafaka mapema kuondoa matatizo yaliyoko nchini mapema ili kuepusha taifa kutumbukia mahala pabaya.Ni jukumu la wabunge bila kujali itikadi zao kupambana kikamilifu kuishurutisha serikali iliyopo kulinda amani na kujali masilai ya walio wengi.

KWELI TANZANIA KUNA AMANI YA KUDUMU?



Wasomaji wangu ni matumaini yangu muu wazima wa afya na mnaendelea vyema na majukumu mbalimbali  ya kujenga taifa na jamii zetu kiujumla.
          Watanzania tumeendelea kuishi kwa amani na furaha huku tukishuhudia ujio wa wakuu wa nchi mbalimbali kuba hapa duniani.Tumeona raisi wa China akiwasili nchini na pia raisi wa Marekani pia amefika nchini na msafara mkubwa. Wote wa hao wamepongeza utawala uliopo tanzania na amani iliyopo.Watawala wa Tanzania wamebaki wakijisifu kwamba wamedumisha utawala bora pengine kuliko nchi nyingine za Afrika.
           Ni wakati wetu watanzania kujiuliza je ni kweli kuna amani ya kudumu Tanzania? Na pia je kuna utawala bora Tanzania?.Haya maswali magumu hayaweyi kujibiwa na viongoyi walioko madarakani bali ni kwa sisi wananchi wa Tanzania kwa kutoa maoni na fikra  zetu.
       Tukianza na utawala bora,mtu akisema utawala bora ina maana ya utawala unaofuata sheria na misingi uongozi na sheria na kanuni za nchi husika.Kwa ripoti mbalimbali na matukio yanayoendelea Tanzania hatuwezi kusema kuna utawala bora nchini.Ufisadi umekua kama hulka  ya viongozi wetu kama ule wa Richmond na dowans ,rada feki naule wa majengo pacha ya BOT.Pia kuna ufisadi na ruswa iliyokisiri katika mahakama zetu,polisi na ngazi mbalimbali za uongozi hapa Tanzania.
             Licha ya ufisadi pia kuna suala la watu kutungiwa kesi za uongo,watu kufungwa muda mrefu bila kufunguliwa mashitaka na matendo mbalimbali ya kupeana ajira na huduma kwa kujuana na ucheleweshaji wa makusudi wa huduma kwa wale raia wenye kipato cha chini.Ni waji bu wa wananchi kupigana kupinga utawala mchafu usio jili matakwa ya wengi
        Kikubwa tulichonacho ni kuendelea kumshukuru mungu kwa kuendelea kutupa amani kwa zaidi ya miaka hamsini sasa.Watanzania wamekuwa wavumilivu na kuendelea kuendelea kutunza amani kwa nguvu zote.Swali linakuja na kuuliza amani hii itadumu mpaka lini?.je watanzania wataendelea kuwa wavumilivu mpaka lini?.Mikono ya sheria imewaona wanao jaribu kuvunja amani kwa nguvu zote?
               Tumeona matukio mbalimbali kama kuuwawa kwa padre kule Zanzibar,bomu kanisani Arusha,Mauaji yaliyo fanywa na polici Arusha,maandamano kule Mtwara na harakati za shehe Ponda.Je haya yote yatanusuru amani iliyopo nchini?.Je ni viashiria tosha vya kutokua na amani mwaka 2015.
          Matatizo yanayoendelea Brazil na Misri yamesababishwa na hali ngumu ya maisha na pia utawala usiojali kama wetu hapa Tanzania.Hivi ni viashiria tosha kwamba kuna kuanguka katika matatizo makubwa siku zijazo.
             Ni rai yangu kwa viongozi wetu kutafuta njia muafaka mapema kuondoa matatizo yaliyoko nchini mapema ili kuepusha taifa kutumbukia mahala pabaya.Ni jukumu la wabunge bila kujali itikadi zao kupambana kikamilifu kuishurutisha serikali iliyopo kulinda amani na kujali masilai ya walio wengi.