Powered By Blogger

Translate

Monday, July 8, 2013

MACHINGA MSIDANGANJIKE


Askari Polisi na Mgambo wa Jiji wakiimarisha ulinzi katika eneo lamanzese jijini Dar es salaam jana, baada ya kutokea vurugu kati ya mgambo na Wamachinga zilizosababisha barabara ya Morogoro kufungwa kwa muda kwa saa tatu. 

Dar es Salaam. Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Jordan Rugimbana amewataka wafanyabiashara ndogondogo (wamachinga) kutodanganywa  na wanasiasa kwa lolote kwani mpango wa kuwaondoa maeneo wasiyotakiwa ni wa lazima. “Leo tunaendelea mitaa ya Manzese, Ubungo na hata Mwenge kwani ni lazima waondoke ili kazi za umma zifanyike’’ alisema.
Kauli ya Rugimbana imekuja ikiwa ni siku moja baada ya kutokea vurugu za wafanyabiashara na polisi wa kutuliza ghasia na mgambo wa jiji waliokuwa wakiwataka kuondoka katika eneo hilo ili kutoa nafasi ya mradi wa ujenzi wa barabara wa mabasi yaendayo kasi (BRT) eneo hilo.
Rugimbana alisema baadhi ya wanasiasa wanatumia majukwaa yao vibaya kwa kuwadanganya wafanyabiashara hao hilo zoezi la kuhamishwa eneo la Manzese ilikuwa ni la muda mfupi kwa ajili ya ujio wa Rais Barack Obama. Akizungumza na Mwananchi kwa simu jana, Rugimbana alisema zoezi la kuwahamisha wamachinga hao ni la kisheria kwa sababu  lazima waondoke ili kumpisha mkandarasi aendelee na ujenzi wa barabara hiyo.
“Tuna mgongano na baadhi ya wanasiasa ndio wanaoturudisha nyuma wanawapotosha hawa wamachinga, sisi tunafuata sheria sio siasa lazima waondoke ili mkandarasi aendelee kufanya kazi eneo lile,” alisema Rugimbana.
Rugimbana  alisema  zoezi hilo ni endelevu hivyo yeyote atakayeenda kinyume na agizo hilo atachukuliwa hatua za kisheria hivyo wametakiwa kuondoka eneo hilo.
Alisema wafanyabiashara hao kama wana matatizo wanatakiwa wamuone mkuu huyo, Meya wa manispaa hiyo ili waweze kukaa pamoja na kutatua matatizo yao.
“Hili zoezi ni endelevu na leo hii oparesheni itaendelea maeneo yote ambayo hayaruhusiwi kama Ubungo, Manzese na Mwenge, kama eneo la Mwenge tumewaondoa wafanyabiashara na vibanda vyao vimebomolewa  ili kupisha upanuzi wa barabara,”

No comments: